Nuzulack Dausen
UKIMUONA kwa mara ya kwanza ni vigumu kufikiri kama anaweza
akawa amepitia katika mikasa migumu ya kutisha ya maisha kama
ilivyomtokea.
Nguo zake kuukuu, nywele za chafu na ulemavu
alionao vinaficha historia nzito aliyonayo katika maisha pamoja na
utaalamu wa kuongea kwa ufasaha lugha za Kiingereza, Kiitaliano na
Kireno licha ya kutosomea.
Huyu ndiye ‘Wa Mbele’ kijana aliyejiwekea ndoto za
kuishi nje hasa Ulaya akiamini kuna maisha mazuri ambayo yangemfanya
naye awe tajiri.
Hata hivyo ndoto zake hizo zilizimika pale hali
hali ilivyobadilika na kujikuta akililia kurudi Tanzania baada ya
kukumbana na mateso, manyanyaso, ukatili na biashara za kuhatarisha
maisha kiasi cha kumfanya awe mlemavu wa viungo vya mwili uliomdhoofisha
na kumharibia maisha yake.
Wa Mbele ambaye jina lake halisi ni Mbembele Said
Lipwata nilikutana naye katika safari yangu Mjini Mtwara. Mbali na
ulemavu wake wa mguu na mkono wa kulia, bado ana uwezo mkubwa wa
kutembea kwa kuruka kwa masafa marefu.
Anasema alizaliwa mwaka 1967 mkoani Mtwara,
alikulia huko hadi mwaka 1976 alipojiunga na elimu ya msingi katika
Shule ya Shangani.
“Hali duni ya maisha ilinifanya nimkimbie baba
aliyekuwa akiishi Mtwara, kwenda kwa mama Magomeni Kagera Jijini Dar es
salaam, niliendelea na masomo yangu huko” anasimulia Mbembele akieleza
kuwa wazazi wake hawakuwa wakiishi pamoja.
Kaka zake wakubwa walikuwa wanajishughulisha na
kazi za ubaharia jambo ambalo lilimpa matumiani makubwa ya kukamilisha
ndoto ambazo alikuwa nazo kwa miaka mingi kwamba siku moja angezamia
kwenda Ulaya akiamini angepata maisha mazuri.
Baada ya kumaliza masomo yake ya msingi mwaka
1983, Mbembele hakuwa na kazi ya kufanya kutokana na kushindwa kuendelea
na masomo ya Sekondari, akaanza kuzunguka na kaka zake katika meli
tofauti ndani ya Pwani ya Afrika Mashariki na kujaribu mbinu za kuzamia
Ulaya.
Majaribio ya kuzamia
Kutokana na kupata uzoefu kidogo katika safari za
meli, Mbembele anasema alianza majaribio ya kuzamia yeye na rafiki zake.
Bandari ya Mtwara na Dar es salaam ndiyo vilikuwa vituo vikuu vya
majaribio yao.