Thursday, February 12, 2015

Zawadi ya pekee kwa mke wangu mtarajiwa siku ya Valentine


Wasalaam kipenzi changu, mke wangu mtarajiwa.
Popote ulipo pokea salamu zangu hizi za dhati zisizo na tone la unafiki. Najua utakuwa umeshtuka kwanini nimekutumia barua hii leo, saa kadhaa kuelekea siku ya Wapendanao ambayo wazungu wanaiita Valentine. Usishtuke, nimekuletea zawadi yako maridhawa, kuwa mtulivu.
Tafadhari, usihudhunike kwa kuwa huna uhakika wa mpenzi au mume kwa sasa. Usisikitike na kujilaani kuwa una kasoro kwa kuwa wenzio wameshaanza pilikapilika za kuandaa au kupokea zawadi mahsusi za Valentine.
Inakuuma kutokuwa miongoni mwa hao thenashara lakini vumilia. Maisha sio maji ya mto yanayofuata mkondo wake. Maisha ni safari na waliombele ndiyo wanaowahi kufika bila kujali wamefika na kupata nini.
Bila shaka ulitegemea kupokea zawadi nzuri za maua mazuri ya waridi yaliyopulizwa manukato yenye rehe nzuri lakini kwa bahati mbaya ni haka kabarua ambako nimesahau kupulizia hata manukato ya ‘Nivea for Men’. Umakini wako kuisoma barua yangu kwa moyo ni zawadi tosha, zawadi nzuri kuliko hata Blackberry, Galaxy Note 4, Vits, IST au safari ya kutembelea visiwa vya Sanane na Zanzibar.
Najua masomo hayaendeki au kazi hazifanyiki huko uliko na unatamani siku ya Valentine iwe fupi, iishe na uachane na ‘mashida’ ya wenzio wanaoweka ‘status’ (ujumbe) mzuri na Selfie na wapenzi wao katika akaunti zao za Whatsapp, Instagram na Facebook.
Tuliza moyo na amini mimi nipo japo hatujawahi kuonana. Futa machozi na usiwaze kulazimisha penzi na mtu ambaye hakupendi, mimi nipo ila wasaa ulikuwa hauujafika wa kuanzisha uhusiano.
Naomba nisikuchoshe sana na maneno ya utangulizi yasiypunguza hata kidogo maumivu ya kovu la kuwa ‘single’ kwa sasa kwa sababu tu yule bepari mwenye gari uliyempenda alikuhadaa kuwa angekuoa lakini kumbe alikuwa na mke na watoto watatu. Au upo single kwa sababu tu vijana wanaoukuja bado hawajielewi au hawajaonyesa nia ya kukuoa na kukucheleweshea kamda kako ka kuolewa.