Thursday, October 13, 2011

Nyerere day iwe chachu ya mabadiliko Bongo

         Ijumaa ya tarehe 14 mwezi huu watanzania tunaadhimisha miaka 12 ya kifo cha Hayati baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere. Siku hiyo Watanzania hatutakuwepo makazini kwa kuwa ni siku ya mapumziko kitaifa. Hii ni siku maalumu kukumbuka kifo cha kiongozi huyu mahiri wa taifa la Tanzania. Siku hii tunahitajika kuzitafakari nasaha za hayati baba wa taifa huku tukimuombea astarehe kwa amani huko alikotutangulia.
Hayati Baba wa taifa Mwalimu Julius K. Nyerere  1922 - 1999
           
            Siku hii si ya kulewa baa au kufanya madhambi kama miongoni mwetu tunavyofikiri. Wengi hutumia siku hii ya mapumziko kwa mambo yao ya ajabu ajabu ambayo baba wa taifa aliyakemea sana kwa kuwa hayana tija katika taifa maskini kama hili. Wakati tukiadhimisha kifo hicho kuna baadhi  yetu wamepanga kutumia siku hiyo kujinufaisha wenyewe. Wapo watu ambao watatumia bajeti iliyopangwa kuwezesha maadhimisho hayo kama mitaji yao binafsi. Na wapo wengine watakao tumia siku hii kufanya mambo yao yasiofaa katika jamii ya kitanzania kama wizi, na masuala mengine ya uvunjifu wa amani.
     Umma wa watanzania lazima utafakari ni changamoto gani tunazipata tangu kuondokewa na kiongozi wetu shupavu JK I. Maadhimisho haya ya miaka 12 ya kifo cha baba wa taifa yanaambatana na maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa Tanzania bara. Je Watanzania tunayaishi aliyotuachia mwalumu? Bila shaka kila mtu anajibu moyoni mwake basi hivyo ndivyo tunavyohitajika kutafakari zaidi ili kutoa mipango bora na endelevu ya kujenga nchi yetu na si ufisadi.
Ni matumaini yangu kuwa watanzania wengi wataitumia siku hii kutafakari kwa kina masuala yote aliyotuachia ba ba wa taifa kama njia moja wapo ya kujenga nchi, Hivyo basi Serikali ihakikishe usimamizi wa kutosha katika maadhimisho hayo. Nyerere day inatuhusu watanzania wote na inabidi tushirikiane kuendeleza kumbukumbu hizi ili zidumu vizazi na viziazi.
      Nawatakia mema katika maadhimisho haya ya kifo cha baba wa taifa!

       

No comments:

Post a Comment