Saturday, February 13, 2016

Wewe ndiye Valentine wangu wa kweli

Nuzulack Dausen
Twitter: @nuzulack
Kwako mke wangu mtarajiwa. Valentine imewadia tena.
Najua bado una huzuni na wasiwasi nimekutelekeza. Una hofu na miaka inavyokwenda kasi bila kunipata mimi, kipenzi chako cha kweli.
Rafiki zako ambao mwaka jana walikuwa waseja kama wewe, tayari wameshaolewa ama kuchumbiwa. Na wewe umeshiriki kikamilifu kuwaoza.
Lakini bado wanisubiri nifike, nije kukuoa licha ya kuwa miaka inazidi kuyoyoma. Hujakata tamaa.
Nafahamu bayana mabarobaro wengi hujipitisha pitisha na kukulaghai uwakubali. Lakini moyo wako u thabiti na hujawapa nafasi. Ndoto yako ya kuwa na mimi imekutawala siku zote.
Mwaka jana nilikusihi usifadhaike wakati wa sherehe za valentine. Nilikusihi usisitetereke na rafiki zako waliokuwa wakiringa kwa zawadi walizopewa na mabwana zao. Mwaka huu pia Valentine inabisha hodi.
Hujapata zawadi yoyote wala ujumbe mzuri kwenye simu yako. Ungetamani umpate mtu wa kukubembeleza ukichoka na kazi na wakati ukiumwa.
Ungetamani uwe na mfalme wa moyo wako ambaye muda wote angekuwa na wewe akikujali na kukupa mapenzi moto.
Kiufupi, unamtaka mume wa kukufanya mke mwema na chaguo la kweli. Lakini bado giza linakuzuia usione nuru. Nuru ya maisha mapya ya kuwa wawili na kutekeleza masharti ya vitabu vya dini.
Tafadhari vumilia.  Hata Valentine hii imefika na hujaniona, usifadhaike. Narudia usikate tamaa. Nipo nakuja japo sijafika karibu yako. Sidhani kama ni Valentine hii lakini utaniona.
Usitishike na rafiki zako wanaokutambishia zawadi za smartphone walizopewa na mabwana wanaotaka kuwachezea. Wala usibabaike na selfie zao wanazoweka mtandaoni wakiweka ‘status’ za “Ready for Valentine (Tayari kwa valentine).”
Mimi ndiyo zawadi yako ya kweli. Zawadi ya kudumu ya maisha yako. Duniani na mbinguni. Upendo wangu kwako ni zaidi ya zawadi ya smartphone au Vitz. Upendo wangu haubanwi na muda eti mpaka siku ya Valentine pekee la hasha. Mimi ni wako siku zote.
Nakupenda kila siku japo hatujawahi onana. Nakuw
aza wakati wote na nakupenda kutokana na uzuri wa asili ulionao, heshima, upole, werevu, ubunifu na uvumilivu wako.
Siyo mapepe wala waruwaru wa kukufanya nyumbani kwetu wakukatae. Huropoki ovyo na kulalamika mara kwa mara mbele za watu hata kama mtu kakukosea mara 1,000. Huvai nguo za vipisi zikakuonyesha maungo yako kana kwamba upo sokoni.
Huweki nyusi za bandia na kujisiliba rangi tofauti usoni ukaonekana kama kichekesho mbele za watu. Hujawahi waza kuweka makalio ya ziada kwa sababu una uhakika mimi situmii maumbo hayo kama kigezo cha mwanamke mzuri.
Hutumi mara kwa mara picha mtandaoni kuonyesha unaponda raha kwa kuwa unajua mwanamke bora hupenda kusitiri mwenendo wa maisha yake binafsi na ya nyumbani.
Hakika wewe ndiyo Valentine wangu. Na mimi ndiyo Valentine wako wa kweli. Nisubiri nije nikupoze moyo. Nivumilie kidogo tu. Nikifika, sitachelewa, nitakutolea posa na kukuoa.
Nikutakie heri ya wapendanao huko uliko japo kila siku hufanya hivyo. Nakupenda mchumba wangu.


Thursday, November 19, 2015

Uwaziri Mkuu wa Majaliwa unavyoweza kujaliwa zaidi

Baada ya Rais John Magufuli kupendekeza jina la Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya awamu ya tano na hatimaye kupitishwa na Bunge, habari zinazozunguka kwa sasa nchini ni kwamba kiongozi huyo mpya ataweza jukumu hilo zito.
Uteuzi wa Majaliwa unaokena kama ni ‘surprise’ kwa Watanzania waliowengi. Ndiyo, huenda kweli ni surprise kwa sababu mwanasiasa huyo si mwingi wa kutafuta ujiko kama wengine.
Inawezekana kweli ikawa Surprise kwa kuwa wengi hawakutarajia kuwa Dk Magufuli angefanya uteuzi wakenje ya miamba ya siasa iliyozoeleka na iliyokuwa ikitajwa kama William Lukuvi na Dk Harrison Mwakyembe.
Kwa aina ya uteuzi huo wa Rais hapana shaka swali la je, Majaliwa atakitendea haki cheo hicho hasa katika Seikali inayojinasibu kwa “Hapa Kazi Tu”, haliepukiki. Na maswali mengi kama hayo yataibuka kila uchwao katika siku hizi za awali ambazo Mbunge huyo wa Ruangwa atakuwa akianza kutekeleza majukumu yake.
Kwa mtazamo wangu, Majaliwa anaweza kwenda na kasi ya Magufuli kwa asilimia 100. Si kwenda nayo yu bali hata kuituliza kasi hiyo pale itakapoonekana kuzidi na kuleta hatari.
Kama mwanahabari nafahamu utendaji wa Majaliwa kupitia nafasi zake alizopitia hasa ya Naibu Waziri wa Ofisi ya Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi (Elimu) ambayo baadhi ya mambo nilikuwa nikiyafutilia kwa karibu likiwemo agizo la rais mstaafu Jakaya Kiwkete la ujenzi wa maabara kwa kila shule ya Sekondari ya Kata.
Hivyo, matokeo ya utendaji bora wa Majaliwa yatachangiwa zaidi na baadhi ya mambo yafuatayo:-

  1. Hafahamiki sana
Licha ya kuwa alikuwa Naibu Waziri katika Serikali iliyopita, Majaliwa siyo miongoni mwa watu maarufu sana kiasi cha mfumo wake wa usimamizi na utendaji kufahamika bayana miongoni mwa watumishi wa umma na wananchi.
Pamoja na kutofahamika sana, Waziri Mkuu ni mtendaji. Ni mtendaji asiyefahamika na wengi. Wengi wanaomfahamu, angalau kasi yake, ni wale waliopo Tamisemi na kwenye sekta ya elimu. Vivyo, wanasiasa wanaoweza kujinadi kuwa wanamfahamu ni wale tu waliokuwa kwenye Kamati mbalimbali za Bunge ambazo zilikuwa zikishirikiana mara kwa mara na Tamisemi.
Sifa hizo zikijumulishwa na uchapakazi wa bosi wake, Dk Magufuli inapatikana picha ya moja kwa moja kuwa watumishi hawatakuwa na njia nyingine zaidi ya kujituma kufanya kazi kutokana na kutojua aina ya misimamo ya Majaliwa.
Matokeo hayo, yatamsaidia vyema mwalimu huyo wa zamani kuwasimamia mawaziri wake ambao bila shaka wengi watakuwa wapya kwenye Baraza la Mawaziri linalotarajiwa kuundwa hivi karibuni.

  1. Presha ya kukilinda chama tawala

Kama ilivyo kwa Rais, Majaliwa naye atakuwa na kibarua kigumu cha kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha anasaidia kuiokoa CCM kutoka madarakani miaka mitano ijayo.
Kwa maana hiyo, hataweza kuruhusu uzembe wowote ndani ya utumishi wa umma ambao huenda ukaipeleka CCM kwenye kaburi la sahau na kuiacha nchi chini ya upinzani.
Ushindani uliokuwepo katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 ni salamu tu kwa Serikali ya JPM ambayo Waziri Mkuu hubeba mizigo kibao ya Serikali pale ufanisi unapopitia mlango wa nyuma.
Hofu hiyo, itasaidia mbunge huyo wa Ruangwa afanikiwe kuitumikia nafasi yake vyema na kuonekana ni mchapakazi na kujibu maswali yanayojitokeza kwa sasa.

  1. Kulinda kibarua chake
Hakuna ubishi kuwa baada ya kuitumikia nafasi hiyo kwa kipindi kifupi, Majaliwa atavutiwa kuendelea kuitumikia ili kibarua kisiote nyasi. Hatakubali kirahisi ibara ya 53A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imng’oe na kuweka historia kwa mara ya kwanza nchini.
Hatothubutu hata kidogo akina Tundu Lissu au Zitto Kabwe waanzishe hoja za kuwa na imani na Waziri Mkuu wakati ana uwezo wa kuzuia hali hiyo mapema kwa kufanya kazi kwa bidii.
Hivyo, nia hiyo njema ya kupalilia kibarua moja kwa moja itamsaidia kuchapa kazi na hata kukwepa vizingiti vya kumwangusha hapo mbeleni.
Kwa vyovyote itakavyokuwa, Majaliwa kama mwanasiasa yoyote anafaa kuwa Waziri Mkuu. Lakini kikwazo kikubwa kinachoweza kumpunguza kasi ni kwamba sehemu kubwa ya utendaji inategemea zaidi mwitikio na ufanisi wa utumishi wa umma. Kama inavyohamika, utendaji wa sekta hiyo unahitaji mabadiliko ya jumla na siyo maboresho ya viraka.
Iwapo watumishi hao watafanya kazi kwa moyo na kuonyesha vipaji vyao bila ya woga wowote Serikali hii itafanikiwa zaidi na kuweka nafasi nzuri zaidi ya kurudi 2020. Ila, ikishindwa ndiyo utakuwa mwisho wake.
Nifuate kupitia Twitter @nuzulack





Monday, May 4, 2015

Wakati wa vijana kuacha mawazo ya kuajiriwa ni sasa


Ni kawaida kwa vijana wengi nchini kuwa na ndoto lukuki za mafanikio wanapoingia vyuo vikuu na vyuo vya kati. Asilimia kubwa huamini kozi wanazochagua na kusomea zitawapatia mafanikio ya haraka zaidi katika maisha.
Dhana hiyo huwafanya kuchagua kozi nzuri ambazo wakihitimu bila shaka watakua mameneja au watu wenye nafasi nzuri zaidi katika kampuni au mashirika makubwa ya umma.
Katika mawazo hayo ya ‘kusadikika’ huwa kuna mipango mingi ya kutekeleza mara baada ya kumaliza elimu zao ikiwamo kupata kazi haraka katika kampuni wanazotarajia kufanya, kuoa au kuolewa na wachache sana huwaza kuwekeza.
Hata hivyo mambo huwa ni magumu pale wanapomaliza stashahada au shahada zao kwa kukosa ajira ambazo huaribu mipango mingine yote. Kwa kiasi kikubwa ajira ndiyo msingi wa mipango mingi ya vijana hivyo ikikosekana kila kitu kinazama.
Nakumbuka hata mimi nilipata wakati mgumu kuchagua kozi ya kusoma kutokana na ushawishi mkubwa niliokuwa na upata kwa wakubwa zangu kuchagua masomo waliyoyaita ya ‘pesa pesa’.
Katika kundi la watu wote waliokuwa wakinishauri hakuna aliyeniambia kuwa nikienda kusoma Mlimani nitumie masomo hayo ili niweze kupata ufahamu wa kuwekeza.

Hakuna aliyethubutu kuniambia kuwa nikiwa shule nitunze fedha kidogo ntakazokuwa napata kwenye mkopo wa elimu ya juu au kutafuta ‘dili’ za muda mfupi zitakazoniongezea kipato kitakachosaidia kuanzisha biashara zangu.
Aina hiyo ya ushauri inazidi kuangamiza asilimia kubwa ya vijana nchini hasa wanaobahatika kupitia vyuo vikuu. Dhana ya kijamaa ya miaka 35 iliyopita ya kupata kazi baada ya chuo bado inatutafuna na kutufanya tuwe watumwa wa ajira.
Vijana wengi tumekuwa waoga wa kujaribu kujiajiri na kujikuta tunabaki mtaani hata baada ya kuhitimu kozi nzuri za biashara. Baadhi yetu hata kabla ya kujaribu kutafuta mawazo ya biashara tunakatishwa tamaa na nafsi zetu kuwa hatuwezi na hakuna vyanzo vya fedha kutuwezesha.
Hofu hiyo kama hiyo ndiyo anayoiita aliyekuwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Ludovick Utouh, kuwa ni matokeo ya kutobadilika ya mawazo ya muda mrefu ya kijamaa. Ni sehemu ya utegemezi wa kufikiri kila kitu kinafanywa na serikali na kuwapatia wananchi mambo mazuri.
Kizazi chetu kimebatika kuishi katika ulimwengu wa habari tele za biashara na uwekezaji lakini ni wachache sana wanaoweza wakatulia na kompyuta zao mpakato au simu wakasoma habari kama hizo.
Aina hiyo ya mawazo itaongeza idadi kubwa ya vijana wasio na ajira ambao baadhi ya wanasiasa wanaliita tatizo hilo kama bomu linalosubiri kulipuka. Iwapo kila mwaka wanahitimu zaidi ya 1 milioni na kuingia kwenye soko la ajira, na asilimia ndogo tu ndiyo wanaajiriwa kuna umuhimu mkubwa kujifunza kuwekeza.
Lakini mawazo na tabia ya kusubiri ajira yanaweza kuondolewa miongoni mwa vijana iwapo tunaweza kufanya yafuatayo;
Mosi, kujenga tabia ya kuwekeza kidogo kinachopatikana wakati tukiwa masomoni. Ni dhahiri kuna baadhi ya vijana wana matatizo ya kifedha lakini pia wapo wenye fedha kidogo zinazoweza kukusanywa taratibu benki pale wawapo masomoni zitakazowasaidia kupata mitaji watakapomaliza vyuo.
Ukikusanya Sh3 milioni kwa miaka mitatu itakayotokana na kuhifadhi kiasi kidogo cha pesa zako na kufanya vibarua bila shaka inaweza kusaidia kuanzisha biashara yoyote itakayosaidia kuishi mjini.
Pili, usomaji wa taarifa mbalimbali utasaidia vijana wengi kupata taarifa za namna ya kuanzisha biashara kutoka kwa watu mbalimbali wenye uzoefu. Binafsi nimejiunga na mtandao kibao inayotoa mafunzo ya ujasiriamali kama yes.com, Forbes, Vijanatz.com, Buni hub na mingine lukuki.
Kwenye vyanzo hivyo vya habari unaweza kupata taarifa nyingi zikiwemo namna ya kupata mitaji kwa kuanzisha mawazo mazuri ya biashara. Kuna wawekezaji lukuki wanatafuta vijana wabunifu watakaokuja na mawazo mazuri ya biashara yatakayoleta faida kubwa kwa mwekezaji na jamii.
Tatu, kuunda mtandao wa vijana wenye malengo ya kibiashara kunaweza kutuepusha na bomu. Vijana tunatakiwa tuwe na uhusiano wa karibu wa kibiashara kwa kuunda mtandao. Aina ya mtandao kama huo unaweza kusadia kuunda wazo, kuwakutanisha na taasisi za kimataifa na za ndani zinazotoa mitaji isiyo na riba kwa njia ya ushindani wa mawazo. Pia, kupitia kikundi ni rahisi kuomba miadi na wajasiriamali wakubwa ili kupatiwa mafunzo ya kutoka kibiashara. Katika soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) kuna wawekezaji lukuki wanaotafuta maeneo ya kuwekeza ila hawajapata mawazo  na kumpuni nzuri za chini na kati.
Mbinu kama hizo zinaweza kuwatoa vijana woga katika kufanya biashara na hatimaye kupunguza idadi ya wanaotegemea ajira. Kama asilimia kubwa ya vijana waliosoma watakuwa wanawaza ujasiriamali basi kuna kila dalili kuwa ajira nyingi zitatengenezwa na kupunguza kundi la wasio na ajira wenye elimu na ujuzi.