Thursday, November 19, 2015

Uwaziri Mkuu wa Majaliwa unavyoweza kujaliwa zaidi

Baada ya Rais John Magufuli kupendekeza jina la Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya awamu ya tano na hatimaye kupitishwa na Bunge, habari zinazozunguka kwa sasa nchini ni kwamba kiongozi huyo mpya ataweza jukumu hilo zito.
Uteuzi wa Majaliwa unaokena kama ni ‘surprise’ kwa Watanzania waliowengi. Ndiyo, huenda kweli ni surprise kwa sababu mwanasiasa huyo si mwingi wa kutafuta ujiko kama wengine.
Inawezekana kweli ikawa Surprise kwa kuwa wengi hawakutarajia kuwa Dk Magufuli angefanya uteuzi wakenje ya miamba ya siasa iliyozoeleka na iliyokuwa ikitajwa kama William Lukuvi na Dk Harrison Mwakyembe.
Kwa aina ya uteuzi huo wa Rais hapana shaka swali la je, Majaliwa atakitendea haki cheo hicho hasa katika Seikali inayojinasibu kwa “Hapa Kazi Tu”, haliepukiki. Na maswali mengi kama hayo yataibuka kila uchwao katika siku hizi za awali ambazo Mbunge huyo wa Ruangwa atakuwa akianza kutekeleza majukumu yake.
Kwa mtazamo wangu, Majaliwa anaweza kwenda na kasi ya Magufuli kwa asilimia 100. Si kwenda nayo yu bali hata kuituliza kasi hiyo pale itakapoonekana kuzidi na kuleta hatari.
Kama mwanahabari nafahamu utendaji wa Majaliwa kupitia nafasi zake alizopitia hasa ya Naibu Waziri wa Ofisi ya Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi (Elimu) ambayo baadhi ya mambo nilikuwa nikiyafutilia kwa karibu likiwemo agizo la rais mstaafu Jakaya Kiwkete la ujenzi wa maabara kwa kila shule ya Sekondari ya Kata.
Hivyo, matokeo ya utendaji bora wa Majaliwa yatachangiwa zaidi na baadhi ya mambo yafuatayo:-

  1. Hafahamiki sana
Licha ya kuwa alikuwa Naibu Waziri katika Serikali iliyopita, Majaliwa siyo miongoni mwa watu maarufu sana kiasi cha mfumo wake wa usimamizi na utendaji kufahamika bayana miongoni mwa watumishi wa umma na wananchi.
Pamoja na kutofahamika sana, Waziri Mkuu ni mtendaji. Ni mtendaji asiyefahamika na wengi. Wengi wanaomfahamu, angalau kasi yake, ni wale waliopo Tamisemi na kwenye sekta ya elimu. Vivyo, wanasiasa wanaoweza kujinadi kuwa wanamfahamu ni wale tu waliokuwa kwenye Kamati mbalimbali za Bunge ambazo zilikuwa zikishirikiana mara kwa mara na Tamisemi.
Sifa hizo zikijumulishwa na uchapakazi wa bosi wake, Dk Magufuli inapatikana picha ya moja kwa moja kuwa watumishi hawatakuwa na njia nyingine zaidi ya kujituma kufanya kazi kutokana na kutojua aina ya misimamo ya Majaliwa.
Matokeo hayo, yatamsaidia vyema mwalimu huyo wa zamani kuwasimamia mawaziri wake ambao bila shaka wengi watakuwa wapya kwenye Baraza la Mawaziri linalotarajiwa kuundwa hivi karibuni.

  1. Presha ya kukilinda chama tawala

Kama ilivyo kwa Rais, Majaliwa naye atakuwa na kibarua kigumu cha kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha anasaidia kuiokoa CCM kutoka madarakani miaka mitano ijayo.
Kwa maana hiyo, hataweza kuruhusu uzembe wowote ndani ya utumishi wa umma ambao huenda ukaipeleka CCM kwenye kaburi la sahau na kuiacha nchi chini ya upinzani.
Ushindani uliokuwepo katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 ni salamu tu kwa Serikali ya JPM ambayo Waziri Mkuu hubeba mizigo kibao ya Serikali pale ufanisi unapopitia mlango wa nyuma.
Hofu hiyo, itasaidia mbunge huyo wa Ruangwa afanikiwe kuitumikia nafasi yake vyema na kuonekana ni mchapakazi na kujibu maswali yanayojitokeza kwa sasa.

  1. Kulinda kibarua chake
Hakuna ubishi kuwa baada ya kuitumikia nafasi hiyo kwa kipindi kifupi, Majaliwa atavutiwa kuendelea kuitumikia ili kibarua kisiote nyasi. Hatakubali kirahisi ibara ya 53A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imng’oe na kuweka historia kwa mara ya kwanza nchini.
Hatothubutu hata kidogo akina Tundu Lissu au Zitto Kabwe waanzishe hoja za kuwa na imani na Waziri Mkuu wakati ana uwezo wa kuzuia hali hiyo mapema kwa kufanya kazi kwa bidii.
Hivyo, nia hiyo njema ya kupalilia kibarua moja kwa moja itamsaidia kuchapa kazi na hata kukwepa vizingiti vya kumwangusha hapo mbeleni.
Kwa vyovyote itakavyokuwa, Majaliwa kama mwanasiasa yoyote anafaa kuwa Waziri Mkuu. Lakini kikwazo kikubwa kinachoweza kumpunguza kasi ni kwamba sehemu kubwa ya utendaji inategemea zaidi mwitikio na ufanisi wa utumishi wa umma. Kama inavyohamika, utendaji wa sekta hiyo unahitaji mabadiliko ya jumla na siyo maboresho ya viraka.
Iwapo watumishi hao watafanya kazi kwa moyo na kuonyesha vipaji vyao bila ya woga wowote Serikali hii itafanikiwa zaidi na kuweka nafasi nzuri zaidi ya kurudi 2020. Ila, ikishindwa ndiyo utakuwa mwisho wake.
Nifuate kupitia Twitter @nuzulack





Monday, May 4, 2015

Wakati wa vijana kuacha mawazo ya kuajiriwa ni sasa


Ni kawaida kwa vijana wengi nchini kuwa na ndoto lukuki za mafanikio wanapoingia vyuo vikuu na vyuo vya kati. Asilimia kubwa huamini kozi wanazochagua na kusomea zitawapatia mafanikio ya haraka zaidi katika maisha.
Dhana hiyo huwafanya kuchagua kozi nzuri ambazo wakihitimu bila shaka watakua mameneja au watu wenye nafasi nzuri zaidi katika kampuni au mashirika makubwa ya umma.
Katika mawazo hayo ya ‘kusadikika’ huwa kuna mipango mingi ya kutekeleza mara baada ya kumaliza elimu zao ikiwamo kupata kazi haraka katika kampuni wanazotarajia kufanya, kuoa au kuolewa na wachache sana huwaza kuwekeza.
Hata hivyo mambo huwa ni magumu pale wanapomaliza stashahada au shahada zao kwa kukosa ajira ambazo huaribu mipango mingine yote. Kwa kiasi kikubwa ajira ndiyo msingi wa mipango mingi ya vijana hivyo ikikosekana kila kitu kinazama.
Nakumbuka hata mimi nilipata wakati mgumu kuchagua kozi ya kusoma kutokana na ushawishi mkubwa niliokuwa na upata kwa wakubwa zangu kuchagua masomo waliyoyaita ya ‘pesa pesa’.
Katika kundi la watu wote waliokuwa wakinishauri hakuna aliyeniambia kuwa nikienda kusoma Mlimani nitumie masomo hayo ili niweze kupata ufahamu wa kuwekeza.

Hakuna aliyethubutu kuniambia kuwa nikiwa shule nitunze fedha kidogo ntakazokuwa napata kwenye mkopo wa elimu ya juu au kutafuta ‘dili’ za muda mfupi zitakazoniongezea kipato kitakachosaidia kuanzisha biashara zangu.
Aina hiyo ya ushauri inazidi kuangamiza asilimia kubwa ya vijana nchini hasa wanaobahatika kupitia vyuo vikuu. Dhana ya kijamaa ya miaka 35 iliyopita ya kupata kazi baada ya chuo bado inatutafuna na kutufanya tuwe watumwa wa ajira.
Vijana wengi tumekuwa waoga wa kujaribu kujiajiri na kujikuta tunabaki mtaani hata baada ya kuhitimu kozi nzuri za biashara. Baadhi yetu hata kabla ya kujaribu kutafuta mawazo ya biashara tunakatishwa tamaa na nafsi zetu kuwa hatuwezi na hakuna vyanzo vya fedha kutuwezesha.
Hofu hiyo kama hiyo ndiyo anayoiita aliyekuwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Ludovick Utouh, kuwa ni matokeo ya kutobadilika ya mawazo ya muda mrefu ya kijamaa. Ni sehemu ya utegemezi wa kufikiri kila kitu kinafanywa na serikali na kuwapatia wananchi mambo mazuri.
Kizazi chetu kimebatika kuishi katika ulimwengu wa habari tele za biashara na uwekezaji lakini ni wachache sana wanaoweza wakatulia na kompyuta zao mpakato au simu wakasoma habari kama hizo.
Aina hiyo ya mawazo itaongeza idadi kubwa ya vijana wasio na ajira ambao baadhi ya wanasiasa wanaliita tatizo hilo kama bomu linalosubiri kulipuka. Iwapo kila mwaka wanahitimu zaidi ya 1 milioni na kuingia kwenye soko la ajira, na asilimia ndogo tu ndiyo wanaajiriwa kuna umuhimu mkubwa kujifunza kuwekeza.
Lakini mawazo na tabia ya kusubiri ajira yanaweza kuondolewa miongoni mwa vijana iwapo tunaweza kufanya yafuatayo;
Mosi, kujenga tabia ya kuwekeza kidogo kinachopatikana wakati tukiwa masomoni. Ni dhahiri kuna baadhi ya vijana wana matatizo ya kifedha lakini pia wapo wenye fedha kidogo zinazoweza kukusanywa taratibu benki pale wawapo masomoni zitakazowasaidia kupata mitaji watakapomaliza vyuo.
Ukikusanya Sh3 milioni kwa miaka mitatu itakayotokana na kuhifadhi kiasi kidogo cha pesa zako na kufanya vibarua bila shaka inaweza kusaidia kuanzisha biashara yoyote itakayosaidia kuishi mjini.
Pili, usomaji wa taarifa mbalimbali utasaidia vijana wengi kupata taarifa za namna ya kuanzisha biashara kutoka kwa watu mbalimbali wenye uzoefu. Binafsi nimejiunga na mtandao kibao inayotoa mafunzo ya ujasiriamali kama yes.com, Forbes, Vijanatz.com, Buni hub na mingine lukuki.
Kwenye vyanzo hivyo vya habari unaweza kupata taarifa nyingi zikiwemo namna ya kupata mitaji kwa kuanzisha mawazo mazuri ya biashara. Kuna wawekezaji lukuki wanatafuta vijana wabunifu watakaokuja na mawazo mazuri ya biashara yatakayoleta faida kubwa kwa mwekezaji na jamii.
Tatu, kuunda mtandao wa vijana wenye malengo ya kibiashara kunaweza kutuepusha na bomu. Vijana tunatakiwa tuwe na uhusiano wa karibu wa kibiashara kwa kuunda mtandao. Aina ya mtandao kama huo unaweza kusadia kuunda wazo, kuwakutanisha na taasisi za kimataifa na za ndani zinazotoa mitaji isiyo na riba kwa njia ya ushindani wa mawazo. Pia, kupitia kikundi ni rahisi kuomba miadi na wajasiriamali wakubwa ili kupatiwa mafunzo ya kutoka kibiashara. Katika soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) kuna wawekezaji lukuki wanaotafuta maeneo ya kuwekeza ila hawajapata mawazo  na kumpuni nzuri za chini na kati.
Mbinu kama hizo zinaweza kuwatoa vijana woga katika kufanya biashara na hatimaye kupunguza idadi ya wanaotegemea ajira. Kama asilimia kubwa ya vijana waliosoma watakuwa wanawaza ujasiriamali basi kuna kila dalili kuwa ajira nyingi zitatengenezwa na kupunguza kundi la wasio na ajira wenye elimu na ujuzi.



Sunday, April 12, 2015

Siasa zitaiangamiza Sumatra, sekta ya Uchukuzi

Moja ya vipindi vigumu kwa Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra) mwaka huu ni hiki inapotakiwa kufanya aumuzi wa kutangaza nauli mpya za usafiri wa umma.
Kwa kipindi cha miezi sita sasa mamlaka hiyo imekuwa aking’ang’anizwa na wadau na viongozi serikalini ishushe nauli kutokana na kushuka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia.
Pamoja na Sumatra kupinga mara kadhaa kuwa mabadiliko yasingefanyika haraka kwa sababu mafuta hushuka na kupaa kwa muda mfupi, wadau hao wakiwemo Baraza la Kutetea Watumiaji wa Uchukuzi (Sumatra CCC) walizidi kuongeza presha ya kushusha nauli.
Sumatra ilishasisitiza kuwa bei ya mafuta inachukua sehemu ndogo tu ya vigezo vya ukokotoaji nauli mpya na zipo gharama nyingine za uendeshaji kama vipuri, bima, mishahara, kodi na mengineyo.
Ni dhahiri kuwa kwa zaidi ya miezi sita wamiliki wa daladala na mabasi ya masafa marefu walipata faida zaidi baada ya kushuka kwa mafuta pasina nauli kushuka na wananchi nao walinyimwa unafuu wa nauli ambao ungesaidia kukuza shughuli zao za kiuchumi.
Tofauti na miaka iliyopita, katikati ya mwaka jana hadi Machi mwaka huu mafuta yalishuka sana kiasi cha Petroli kufikia Sh1,650 jijini Dar es Salaam, bei ambayo ilifikiwa miaka minne iliyopita.
Baada ya mashinikizo, Sumatra ilianza kukusanya maoni ya wadau kama sheria inavyowataka ili kupata mitazamo tofauti ya kutekeleza zoezi hilo.
Katika mkutano uliofanyika Dar es Salaam Machi 18, wamiliki daladala walipinga ushushaji nauli wakihofia mafuta yangepanda bei zaidi na wakatishia iwapo nauli itashushwa, wataanzsisha nauli kwa askari wa majeshi yote.
Wakati Sumatra ikiyafanyia kazi maoni na kufuatilia hali ya soko, Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta wiki iliyopita aliigiza tena mamlaka hiyo kuharakisha majadiriano na wadau na kisha kutangaza nauli mpya ndani ya juma hilo. Hata hivyo, mpaka sasa nauli mpya hazijatangazwa.
Presha kama hizo ni changamoto na kipimo cha uweledi na ufanisi kwa mamlaka za udhibiti nchini. Kuna kila dalili pia kuwa Sumatra inahofia kufanya uamuzi huo isionekane ya ‘kijinga’ na isiyofuata uweledi kutokana na hali halisi ya soko dhidi ya siasa.
Kama Wachumi wengi walivyoonya awali, bei ya mafuta imeanza kupanda tena hata kabla ya nauli mpya kutangazwa. Petroli mwezi huu, Dar es Salaam inauzwa Sh103 zaidi ya bei ya Machi ya Sh1652. Dizeli imepanda kwa Sh109 na Mafuta ya Taa kwa Sh132.
Shilingi nayo imezidi kuporomoka kutokana na kuongezeka thamani ya Dola ya Marekani ulimwenguni na sasa Dola moja inabadilishwa kwa Sh1, 850. Vipuri na mabasi huingizwa nchini na wafanyabiashara wake huathiriwa sana na udhaifu wa thamani ya Shilingi.
Hali ya kisiasa mwaka huu inayohusiana na Uchaguzi Mkuu inaweza kuathiri mwenendo wa kiuchumi kutokana na wawekezaji wengi kuhofia hatari za kiuwekezaji na mabadiliko ya kiutawala yanayoweza kutokea.
Pia, kuna kila dalili bei ya mafuta ikazidi kupanda. Takwimu za Benki ya Dunia (WB) zinaonyesha wastani wa bei ya mafuta ghafi katika soko la dunia kwa mwezi Februari iliongezeka hadi Dola za Marekani 54.93 (Sh101, 600) kwa pipa kutoka bei ya chini kuliko zote kwa miaka mitano ya Dola 47.45 (Sh87,780) kwa pipa mwezi Januari mwaka huu.
Ripoti ya Machi, 2015 ya nchi zinazozalisha mafuta sana ulimwenguni (Opec) inaonyesha mahitaji ya mafuta duniani mwaka huu yataongezeka kwa mapipa 1.17 milioni kwa siku na kufanya wastani wa mahitaji ya jumla kwa siku kuwa mapipa 92.37 milioni. Hii itapandisha bei ya nishati hiyo licha ya Marekani na Canada kwa kuzalisha mafuta mepesi mengi zaidi kwa bei ndogo.
Kwa mantiki hiyo na ukiachana na siasa, uamuzi wa Sumatra kushusha nauli ni mtego usiofanana hata kidogo na kipindi cha mabadiliko ya nauli mwaka 2009.
Iwapo Sumatra italazimishwa, itaingia kwenye mgogoro na wasafirishaji na kuwapa wananchi ahueni ya muda mfupi tu.
Mfumo mzuri na wa haraka wa ukokotoaji nauli uendao na soko ni kama unaotumika na Ewura kukotoa bei ya mafuta kila mwezi. Huo ungewaepusha Sumatra na kadhia na presha za kisiasa.
Sumatra ingekuwa inapitia nauli angalau kwa miezi sita au mwaka kuepusha unyonyaji kama ulitokea hivi karibuni kwa wananchi kwa kushindwa kushusha nauli haraka kwa mujibu wa mwenendo wa soko la mafuta.
Nuzulack Dausen ni mwandishi wa gazeti la Mwananchi anapatikana kupitia ndausen@tz.nationmedia.com au Twitter: @nuzulack






Thursday, February 12, 2015

Zawadi ya pekee kwa mke wangu mtarajiwa siku ya Valentine


Wasalaam kipenzi changu, mke wangu mtarajiwa.
Popote ulipo pokea salamu zangu hizi za dhati zisizo na tone la unafiki. Najua utakuwa umeshtuka kwanini nimekutumia barua hii leo, saa kadhaa kuelekea siku ya Wapendanao ambayo wazungu wanaiita Valentine. Usishtuke, nimekuletea zawadi yako maridhawa, kuwa mtulivu.
Tafadhari, usihudhunike kwa kuwa huna uhakika wa mpenzi au mume kwa sasa. Usisikitike na kujilaani kuwa una kasoro kwa kuwa wenzio wameshaanza pilikapilika za kuandaa au kupokea zawadi mahsusi za Valentine.
Inakuuma kutokuwa miongoni mwa hao thenashara lakini vumilia. Maisha sio maji ya mto yanayofuata mkondo wake. Maisha ni safari na waliombele ndiyo wanaowahi kufika bila kujali wamefika na kupata nini.
Bila shaka ulitegemea kupokea zawadi nzuri za maua mazuri ya waridi yaliyopulizwa manukato yenye rehe nzuri lakini kwa bahati mbaya ni haka kabarua ambako nimesahau kupulizia hata manukato ya ‘Nivea for Men’. Umakini wako kuisoma barua yangu kwa moyo ni zawadi tosha, zawadi nzuri kuliko hata Blackberry, Galaxy Note 4, Vits, IST au safari ya kutembelea visiwa vya Sanane na Zanzibar.
Najua masomo hayaendeki au kazi hazifanyiki huko uliko na unatamani siku ya Valentine iwe fupi, iishe na uachane na ‘mashida’ ya wenzio wanaoweka ‘status’ (ujumbe) mzuri na Selfie na wapenzi wao katika akaunti zao za Whatsapp, Instagram na Facebook.
Tuliza moyo na amini mimi nipo japo hatujawahi kuonana. Futa machozi na usiwaze kulazimisha penzi na mtu ambaye hakupendi, mimi nipo ila wasaa ulikuwa hauujafika wa kuanzisha uhusiano.
Naomba nisikuchoshe sana na maneno ya utangulizi yasiypunguza hata kidogo maumivu ya kovu la kuwa ‘single’ kwa sasa kwa sababu tu yule bepari mwenye gari uliyempenda alikuhadaa kuwa angekuoa lakini kumbe alikuwa na mke na watoto watatu. Au upo single kwa sababu tu vijana wanaoukuja bado hawajielewi au hawajaonyesa nia ya kukuoa na kukucheleweshea kamda kako ka kuolewa.