Monday, January 21, 2013

SEKRETARIETI YAANZA KUFANYA UHAKIKI WA MALI NA MADENI YA VIONGOZI WA UMMA


Nuzulack Dausen

WITO umetolewa kwa mwananchi yeyote mwenye taarifa za mali za viongozi wa umma nchini kupeleka taarifa hizo kwa Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Umma ili kusaidia zoezi la uhakiki wa rasilimali na madeni ya viongozi hao.

 Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma inatarajia leo kuanza zoezi la uhakiki wa rasilimali na madeni  ya viongozi wa umma mpaka tarehe 15 februari mwaka huu.

Hayo yamesemwa katika taarifa iliyotolewa mwishoni mwa juma lililopita na Kamishna wa maadili ya viongozi wa umma Jaji Mstaafu Salome Kaganda iliyoomba ushirikiano wa karibu kati ya wadau na Sektetarieti katika kukamilisha zoezi hilo.

“Wito unatolewa kwa mwananchi yeyote mwenye taarifa za mali za viongozi hao anaweza kuwasilisha taarifa hizo kwa kamishna wa maadili” alisema Jaji Kaganda.

Zoezi hilo la uhakiki linatarajiwa kufanyika nchi nzima ambapo litahusisha viongozi wote kutoka katika mihimili mitatu ya dola yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

 “Wakati wa uhakiki watendaji wa Sekretarieti ya Maadili watatembelea maeneo ziliko mali za viongozi wakiwa na wathamini(valuers) ili kuthamini mali hizo kwa lengo la kujiridhisha na usahihi wa taarifa za mali walizowasilisha kwa Kamishna wa Maadili” alisema Jaji Kaganda.

Alisema taratibu zote za uhakiki wa rasilimali hizo zilishafafanuliwa katika barua za viongozi ambao watahusika katika zoezi hilo awamu hii.

Aidha, Jaji Kaganda aliwatahadharisha viongozi hao kuwaepuka matapeli ambao wanaweza kujifanya ni watendaji wa sekretarieti ya maadili ili kujinufaisha.

“Sekretarieti inawaomba wadau mbalimbali ushirikiano na pia kuwakumbusha kuwa makini na baadhi ya watu wanaoweza kujifanya ni watendaji wa sekretarieti ya Maadili kwa lengo la kujinufaisha” alibainisha Jaji Kaganda.

Aliendelea kusema kuwa endapo viongozi hao watakuwa na mashaka juu ya mwenendo wa mtu yeyote wawasiliane na sekretarieti ya maadili kwa ufafanuzi zaidi.

“Ieleweke wazi kwamba uhakiki ni zoezi la kawaida na watakaohusika na uhakiki huo hawana tuhuma ya aina yeyote ile. Viongozi wanatakiwa kutoa ushirikiano  kwa maafisa wa sekretarieti wa uhakiki huo” aliongeza Jaji Kaganda.

No comments:

Post a Comment