Saturday, November 17, 2012

Dk Nagu ahimiza uchangiaji wa Mabweni ya Wasichana



WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji na Uwezeshaji Dk Mary Nagu jana aliongoza mamia ya wananchi katika matembezi ya hisani ya kuchangia ujenzi wa mabweni ya wasichana yaliondaliwa na mamlaka ya Elimu nchini (TEA) na kudhaminiwa na Cokacola yaliyoanzia Mlimani city na kumalizika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es salaam.

Dk Nagu alichangisha kiasi cha zaidi ya Sh 13 milioni  na kufanya jumla ya michango iliyokusanywa kuwa Sh 50 milioni ambayo inakaribia kufikia lengo la kukusanya Sh 78 milioni ambazo zitasaidia ujenzi wa mabweni  30 ya shule 8 za Sekondari zilizochaguliwa kuanza na mpango huo maalumu wa kuwasaidia watoto wa kike kutokana na kuwa na mazingira magumu sana.

 Katika hotuba yake aliyoitoa kwenye matembezi hayo Dk Nagu alisema kuwa ni kipindi kirefu sana watoto wakike wamekuwa wakikosa elimu kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kihistoria kama kunyimwa kusoma, ndoa na mimba za utotoni lakini serikali pamoja na wadau wa elimu wameendelea kushirikiana kuhakikisha hali inabadilika kwa  haraka.

Alisema kuwa ili kuendelea kukabiliana na changamoto hizo vyombo husika na kila mtanzania anahitajika kuchangia na kukemea vitendo vinavyorudisha nyuma maendeleo ya elimu ya mtoto wa kike ili kutokomeza janga hilo.
“Natoa wito kwa vyombo vinavyopaswa kuwachukulia hatua wahusika wa uharibifu huu watimize wajibu wao wa kuhakikisha watoto wa kike wanapata haki yao ya kikatiba ya kupata elimu bora bila kubughuziwa” alisema Waziri Nagu.

 Waziri wa ofisi, waziri mkuu uwekezaji na uwezeshaji Dk. Mary Nagu katikati, akiteta jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka wa Elimu Rosemary Lulabuka wa pili kutoka kushoto wakati wa matembezi ya hisani kuchangia mabweni ya wasichana.  Kushoto ni Naibu  Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu na kulia ni Mariamu Ndaba na wa pili kutoka kulia ni Mwenyekiti wa bodi ya mamalaka ya elimu Dk Naomi Katunzi.
  
Aidha aliwashauri wanafunzi wa kike kujidhatiti na kuacha kurubuniwa na vitu vidogovidogo vinavyoweza kuwaharibia maisha yao ya baadaye na kuongeza kuwa ni bora wakatumia muda wao wa masomo vizuri ili wasijutie hapo baadaye watakaposhindwa kutimiza ndoto zao za kielimu.
Waziri Nagu aliviomba vyombo vya habari kuhamasisha uchangiaji wa ujenzi wa mabweni hayo na kusema kuwa watangaze na kuandika sana kama walivyoandika habari zake za ushindi wa Nec.

Katika matembezi hayo Waziri Nagu alichangia kiasi cha sh 1 milioni na kuahidi kuwa atatumia muda wake wa wiki nzima  kuhamasisha uchangiaji zaidi wa ujenzi wa mabweni hayo ya wanafunzi wa kike.

Vilevile katika matembezi hayo walioambatana na Waziri Nagu ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyarandu na mke wake Faraja Nyarandu, Mwenyekiti wa bodi ya Mamlaka ya elimu Dk Naomi Katunzi na Mabalozi  wa uchangiaji huo Msanii Barnaba na Rebeca Gyumi wakiongozwa na mwenyeji wao Mkurugenzi Mkuu wa TEA Rosemary Lulabuka ambapo Naibu Waziri Nyarandu na familia yake walichangia Sh 10 milioni.

Waziri wa ofisi, waziri mkuu uwekezaji na uwezeshaji Dk. Mary Nagu katikati akiwa na Dk Naomi katunzi wa pili kushoto na naibu  Naibu  Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu kushoto. Kutoka kulia ni Rebeca Gwumi Balozi wa Kampeni , Mariamu Ndaba na Mkurugenzi Mkuu wa TEA Rosemary Lulabuka. Waliosimama nyuma kutoka Mabalozi wa kampeni hiyo akiwemo Faraja Nyarandu wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kuhitimisha matembezi ya hisani ya kuchangia ujenzi wa mabweni ya wasichana.
Wakati huo huo Mwanafunzi Hadija Nuru wa Shule ya Sekondari Baobab aliwaomba  na kushauri TEA wapanue wigo wa uchangiaji kwa kufanya bahati nasibu na kuongeza kuwa ujenzi wa mabweni hayo uambatane na uwepo wa huduma za afya, maji, umeme na nyumba za walimu na kufanya ukarabati wa majengo hayo kila wakati itakapohitajika  ili kuyadumisha zaidi.

Barnaba naye afunguka 
Msanii wa muziki wa kizazi kipya Barabas Elias naye alifunguka katika matembezi hayo na kusema kuwa wasanii waote wenye sauti kama yake waanze kujihusisha na masuala ya kijamii kama anavyofanya yeye kwa kuwa balozi wa kampeni za kuchangia ujenzi wa mabweni ya wasichana.

Barnaba wa pili kutoka kulia akitumbuiza na wasanii wenzake wa THT wakati wa hitimisho la matembezi ya hisani ya kuchangia ujenzi wa mabweni.
Alisema kuwa wasanii kama Diamond, Amin, Linna na wengineo wanaweza wakapanga muda wao japo kidogo kuchangia kidogo ili kuwasaidie wasichana ha waendelee na elimu zaidi.

Barnaba aliburudisha umati wa wanafunzi na wadau wengine waliokuwepo kwa kuipa nyimbo zake mabalimbali kama Magumegume, Sijutii niliyempata na zingine zilizotamba kwa vipindi vyote.

Hata hivyo Barnaba aliimba wimbo wa Linnah "angalau nina furaha" kama ishara ya kumshirikisha mwanamziki huyo kwenye ubalozi huo na pia kama heshima ya mtoto wa kike.






Barnaba akiwahamasisha wanafunzi walioshiriki matembezi hayo kucheza kwaito, mbele kulia  mwenye miwani  ni Miss wa zamani Faraja Kota mabaye sasa ni mke wa Naibu waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyarandu.


Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Jangwani wakifuatilia shoo ya Barnaba.





No comments:

Post a Comment